Tukitambua Kifungo cha 7 cha Katiba ya Kenya kimebainisha lugha ya Kiswahili ni lugha pek…
Motion text
KWAMBA, tukitambua Kifungo cha 7 cha Katiba ya Kenya kimebainisha lugha ya Kiswahili ni lugha pekee ya kitaifa, na pia ni lugha rasmi, pamoja na Kingereza katika nchi ya Kenya, aidha Serikali imepewa wajibu wa kulinda na kuendeleza lugha tofauti za watu wa Kenya, na kukuza matumizi ya lugha za kiasili nchini; tukitanabahi kwamba Kiswahili ni mojawapo wa lugha rasmi za Umoja wa Nchi za Afrika, na pia Vifungo vya 119 na 137 vya Mkataba wa Uanzilishi wa Jumuia ya Afrika Mashariki vimewajibisha dola za Afrika Mashariki kustawisha na kuendeleza lugha ya Kiswahili kama lugha ya umoja katika nchi za Afrika Mashariki; tukifahamu kwamba nchi ya Tanzania iliunda Baraza la Kiswahili la Kitaifa (BAKITA) katika mwaka wa 1967, na pia Zanzibar ikabuni Bazara la Kiswahili la Zanzibar (BAKIZA) katika mwaka 2004, kwa madhumuni ya kukuza, kuimarisha na kuendeleza mbele lugha ya Kiswahili katika Tanzania bara pamoja na visiwa vya Zanzibar; tukitambua kwamba mkutano wa tatu wa Baraza la Mawaziri wa Kenya uliofanyika tarehe 14 Agosti 2018 iliidhinisha kuanzishwa kwa Baraza Kuu ya Kiswahili ya Kitaifa kuambatana na Kifungu cha 137 cha Mkataba wa uanzilishi wa Jumia ya Afrika Mashariki; ikifahamika kwamba Kiswahili ni lugha ya kiasili kwa jamii za mkoa wa pwani nchini Kenya, na pia idadi kubwa ya Wakenya ni wazungumzaji wa lugha ya Kiswahili; tukijua kwamba lugha ya Kingereza ina nguvu sana katika mawasiliano rasmi, na kwa hivyo kuchangia kudhofika kwa lugha yetu ya Kiswahili; tukitambua uamuzi wa Baraza la Mawaziri kuhusu kubuniwa kwa Halmashauri Kuu ya Kiswahili ya Kitaifa bado haujatekelezwa; Kwamba, Bunge hili linahimiza Serikali Kuu kupitia Wizara ya Michezo, Utamaduni na Urithi kuanzisha rasmi Baraza Kuu ya Kiswahili ya Kitaifa na kuzindua mikakati, mbinu na sera makhusisi zinazohitajika kukuza na kuendeleza lugha ya Kiswahili, na kushirikiana na vyombo vingine vya kitaifa na vya kibinasi vinavyohusika na uboreshaji wa lugha ya Kiswahili.
Tracker remarks
Hoja kukubaliwa
Source: parliament.go.ke. Last updated 5 Jul 2026.